DC MJEMA AENDELEA KUNG’ARA MBIO ZA MWENGE WA UHURU
Mkuu wa Mkoa wa DSM Mhe. Paul Makonda akimkabidhi Mwenge wa Uhuru Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe. Paul Makonda, tayari kukimbizwa katika Wilaya ya Ilala


Na Mwandishi wenu,Dar es salaam
Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe. Sophia Mjema, leo Julai 07, 2018, ameupokea Mwenge wa Uhuru kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Paul Makonda, na kuukimbiza katika Wilaya yake ya Ilala kupitia jumla ya Miradi 6 ya maendeleo ambayo 3 imewekewa jiwe la Msingi, 1 umekaguliwa na 2 imefunguliwa. Miradi hiyo ni pamoja na Ujenzi wa Daraja la Kivule ambalo liko hatua za mwisho kukamilika, Ujenzi wa Hosteli za wanafunzi wa kike katika shule ya Sekondari Mbondole ambazo zimejengwa kwa fedha za Halmashauri, Ujenzi wa madarasa 3, Ofisi ya utawala na ununuzi wa thamani katika shule ya Msingi Gogo, Uzinduzi wa Hospitali ya Miracolo, Ukaguzi wa Jengo la Mradi wa DMDP na Uzinduzi wa Mradi wa Choo cha mtoto wa Kike katika shule ya Msingi Ilala. Miradi hii yote ina thamani ya Shilingi Bilioni 4.3 zinazotokana na Halmashauri, serikali kuu, wananchi na wadau mbalimbali.
Akizungumza na wananchi wa Ilala ambao walijitokeza kwa wingi kuulaki na kuushangilia Mwenge huo, kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru 2018 ndugu Charles Francis Kabeho aliipongeza Wilaya ya Ilala kwa kazi kubwa iliyofanyika ya kufanya uwekezaji katika elimu hasa Ujenzi wa miundombinu ya Elimu ambayo itaboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia ili kuinua kiwango cha ufaulu Wilayani humo. Aidha, aliwataka wananchi kutimiza wajibu wao wa kununua mahitaji ya Msingi kwa watoto wao yakiwemo daftali, viatu na sare za shule kwani serikali ya awamu ya tano Chini ya Rais wetu Mzalendo Mhe. Dr. Magufuli imeamua kutoa elimu bila malipo, ili kila Mtoto asiikose fursa hii ya kupata elimu.

Aidha ndugu Charles Kabeho ameagiza Mkandarasi anayejenga daraja la Kivule kukatwa fedha anazotakiwa kulipwa endapo hatakamilisha Ujenzi wa Daraja hilo kwa wakati.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe. Sophia Mjema aliwashukuru wananchi wote na kuahidi kuendelea kuisimamia miradi hiyo iliyopitiwa na mbio za Mwenge na miradi mingine ili kuhakikisha kwamba thamani ya fedha inazingatiwa katika ujenzi wa miradi mbalimbali inayoendelea wilayani humo.
Kesho Mwenge wa Uhuru utakabidhiwa kwa Wilaya ya Kigamboni kuendelea na mbio hizo katika mkoa wa Dar es salaam. Katika Mashindano ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2017, Wilaya ya Ilala ilishika nafasi ya kwanza Mkoa wa Dar es salaam, kwa kukidhi vigezo vilivyoanishwa katika muongozo wa Mbio za Mwenge.
Safi
ReplyDelete